• Breaking News

    Friday, 6 January 2017

    Kuhamisha Makaburi


    Suali;
    Je katika uislamu kuhamisha makaburi kunaruhusiwa? na ni nini mtizamo wa uislamu juu ya swala hili la uhamishaji makaburi. Tafadhali nitajie masharti ya uhamishaji makaburi kama kunakubalika.
                  Wabillahi taufiiq.

    Majibu;
    Maulamaa wamekubaliana kuwa ni haramu kufukuwa na kuhamisha maiti au kuzika maiti ndani ya kaburi la maiti mwingine isipokuwa kama mwili wote pamoja na mafupa ya maiti aliyezikwa humo yashatoweka nakugeuka mchanga.
    Ikibaki sehemu yoyote ya mwili wa maiti aliyezikwa humo basi haijuzu kuzika ndani yake wala kuihamisha maiti hiyo. Lakini maiti ikeshageuka na kuwa mchanga basi hapo inajuzu kuzika maiti nyingine ndani ya kaburi hilo.

    Anasema Sayed Sabeq katika 'Fiqhul Sunnah' kuwa madhehebu ya Maimamu Malik na Shafi na Hanbali wanakubali kufukuliwa kaburi iwapo maiti amezikwa na mali au hajaelekezwa kibla kama ilivyosimuliwa na Abu Daud kutoka kwa Abdullah bin Omar (RA) kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) aliruhusu lifukuliwe kaburi la Abu Raghal kwa sababu alizikiwa akiwa na dhahabu.
    Madhehebu hayo yanakubali pia kufukuliwa maiti iwapo amezikwa bila kuoshwa isipokuwa kama panahofiwa isije maiti hiyo ikavurugika.

    Kuhamisha Maiti;
    Ama kuhamisha maiti kutoka katika makaburi yao na kuyapeleka kuyazika ndani ya makaburi megine, hiyo maulamaa wote wamesema kuwa ni haramu isipokuwa panapo dharura kubwa sana au kwa manufaa ya watu kama vile kupanua barabara kutokana na watu kudhikika au kwa ajili ya kupanua ardhi kwa ajili ya kilimo nk. na hii sharti maiti ziwe zishageuka kuwa mchanga, kwani haijuzu kufukuwa makaburi wakati maiti bado mbichi kwa kuhofia yasije yakavurugika na kuchanganyika au kukatikakatika.
    Wallahu taala aalam.

    No comments:

    Post a Comment

    Fashion

    Beauty

    Culture