• Breaking News

    Friday, 6 January 2017

    Swali na JIbu

    Assalam alaykum
    Suali ambalo kwa muda mrefu linanisumbuwa ni je Swala inakuwa haipandi kama ukiwaza ndani yake. Kila siku najaribu nisiwaze katika swala lakini najikuta nikiwaza bila ya kutarajia. Nimefikia hata ya kutia nia ya kutowaza mapema zaidi tangu wakati wa kutia udhu lakini haijasaidia.
    Najua hii ni kazi ya ibilisi lakini sijui nimuepuke vipi kwani najaribu kufikiria kwamba Mungu yuko mbele yangu, na pia kukumbuka kwamba kila nikisoma suratul_Fat-ha Yeye hujibu
    Naona M/Mungu hatoridhika ikiwa sijaweza kuituliza Swala yangu. Mungu anizidishe subira labda nikiendelea kuomba kuwa mnyenyekevu nitafanikiwa kuinusuru swala yangu. Naomba nasaha juu ya tatizo hili kwani nahofia kwamba swala zangu zitakuwa hazina thamani.  
    Jazaka Allah Kheri

    Majibu:
    Wa alaykumussalaam wa Rahmatullahi wa Barakatuh
    Mwenyezi Mungu akujaze kila la kheri katika kuchunga kwako huku na kutaka Swala yako iwe kamili.
    Kutokana na kauli za maulamaa mbali mbali; Swala yako ni sahihi ikiwa unazitimiza nguzo na fardhi zote za swala, isipokuwa tu usiache kuendelea kushindana na shetani mpaka utakapoweza kumshinda Inshaallah.
    Endelea kutafakari juu ya aya unazozisoma, kutafakari unapofanya takbiyr na tasbiyh, na daima jaribu kukumbuka kuwa upo mbele ya Mola wako Subhanahu wa Taala na kwa ajili hiyo lazima uishughulishe nafsi yako kwa ajili Yake tu. Na pia usiache kumuomba Mwenyezi Mungu akusaidie kabla ya kuanza kusali na kila unapoomba dua.
    Waliulizwa Masheikh Ibnu Baz na Sheikh Ibn Uthaymiyn juu ya jambo hilo wakajibu ifuatavyo:
    "Hukmu ya jambo hili mtu anapokuwa ndani ya Swala na wakati mkubwa wa sala hiyo anakuwa katika kutafakari mambo ya kidunia au hata katika mambo ya dini, wanavyuoni wengi wanaona kuwa Swala yake ni sahihi, na kwamba fikra zake hizo hazimbatilishii Swala yake, isipokuwa anapunguziwa thawabu za sala hizo."
    Kwa ajili hiyo inampasa mwanadamu ajaribu kadiri anavyoweza kuuhudhurisha moyo wake uwe ndani ya Swala tu, kwa sababu hiyo ndiyo khushuu, na khushuu ndiyo msingi wa Swala.

    No comments:

    Post a Comment

    Fashion

    Beauty

    Culture