Suali;
Vipi mtu anailipa
raka-a aloisahau anapokuwa ndani ya Sala au akeshamaliza?
Jawabu;
Mtume (SAW) anasema;
"Mmoja wenu akitia
shaka katika Sala yake, akawa hana hakika amesali raka-a moja au mbili, basi
atajaalia kuwa amesali raka-a moja (tu). Na akiwa hana hakika amesali raka-a
mbili au tatu, basi atajaalia kuwa amesali raka-a mbili, na akiwa hana hakika
amesali tatu au nne, basi atajaalia kuwa amesali raka-a tatu, kisha atasujudu
sajda mbili akishamaliza kusali kabla ya kutoa salamu akiwa bado amekaa."
Ahmed na Ibni Majah na
Attirmidhiy.
Na katika hadithi
nyingine anasema Mtume (SAW);
"Mmoja wenu akitia
shaka katika Sala yake akawa hajui amesali (raka-a) ngapi, tatu au nne, basi
aondoe shaka na ahesabu zile raka- ambazo ana hakika nazo (yaani tatu) kisha
asujudu sajda mbili kabla ya kutoa salam. Ikiwa atakuwa amesali raka-a tano,
basi (sajda) zitamtakasia Sala yake, na ikiwa amekamilisha nne basi (sajda)
zitamdhalilisha shetani."
NAMNA NA KULIPA RAKA-A
Kutokana na haya
tunaelewa kuwa raka-a iliyosahauliwa, au yenye kutiliwa shaka inalipwa kama
ifuatavyo;
Kwa mfano ikiwa mtu
anasali sala yenye raka-a nne, na akishafika raka-a ya nne akatia wasi wasi ni
raka-a ngapi amesali, tatu au nne, basi atajaalia kuwa amesali raka-a tatu zile
alizo na uhakika nazo, kisha anaongeza ya nne na anapomaliza na kabla ya kutoka
salamu anasujudu sajda mbili kisha anatoa salamu bila kusoma tahiyatu.
Ipo hitilafu baina ya
maulamaa. Wapo wanaosema kuwa sajda ni baada ya kutoa Salamu hasa kwa Imamu,
kwani akisujudu baada ya salamu atawababaisha wanaosali nyuma yake wale
waliochelewa kwa sababu watainuka mara baada ya kutoa salamu.
Zipo dalili
zinazotujulisha kuwa mtu anaweza kuilipa raka-a aliyoisahau au alizozisahau wakati
wowote ule hata kama
ataikumbuka baada ya kutoa salamu na baada ya kuzungumza, au hata kama
ataikumbuka baada ya kurudi nyumbani au hata baada ya kupita muda mrefu.
Na wengine wanasema
kuwa ukishapita muda wa kiasi cha kusabih, basi itambidi azisali tena raka-a
zote kwa ukamilifu.
Imepokelewa kuwa siku
moja Mtume (SAW) alisahau akapunguza katika sala ya raka-a nne akasali mbili tu
kisha akatoa salamu. Mtu mmoja aitwae 'Dhul yadayni' akamuuliza;
"Ewe Mtume wa
Mwenyezi Mungu! Umesahau au umepunguza kusudi katika Sala?"
Mtume (SAW) akasema;
"Sikusahau wala
sikupunguza (kwa makusudi)."
Kisha akawauliza
Abubakar na Omar;
"Ni kweli
anayosema Dhulyadayani?"
Wakasema;
"Ni kweli."
Mtume (SAW) akainuka na
kuikamilisha Sala, kisha akatoa salamu, kisha akasema 'Allahu akbar', na kusujuu
sajda mbili.
Bukhari na Muslim
No comments:
Post a Comment