• Breaking News

    Friday, 6 January 2017

    Sumayyah bint Khayaat - Shahidi wa kwanza Katika Uislamu

    Hiki ni kisa cha kusikitisha, cha kufundisha na cha kuzingatia na kinaanzia kwa aliyekuwa mumewe Yaasir. Yaasir akiwa pamoja na ndugu zake wawili  walitoka Yemen kuelekea Makkah kwa lengo la kumtafuta ndugu yao aliyepotea kwa miaka mingi.

    Jitihada yao haikuweza kuzaa matunda na baada ya kuchoka wakaamua kurudi kwao Yemen isipokuwa Yaasir ambae alipendezewa sana na mji wa Makkah na akaamua kubakia hapo.

    Ilikuwa ni kawaida ya wageni kutafuta mwenyeji wa kumpa himaya na hivyo Yaasir akapatiwa himaya na Abu Hudhayfah ibn Al Mughiyrah Al Makhzuumiy ambae alikuwa na kijakazi aliyekuwa akiitwa Sumayyah.

    Baada ya kupita muda Sumayyah aliolewa na Yaasir na wakapata mtoto wao wa kwanza aliyeitwa ‘Ammaar. Abu Hudhayfah alimwachia huru kijakazi wake Sumayyah na wakaendelea kuwa na mahusiano mazuri kati yao. Pia walijaaliwa watoto wengine wawili Abdullah na Harith. Abdullah alifariki kabla ya kuja Uislamu.

    Ilipotangazwa dini ya haki iliyovunja ibada za kijahiliya katika mji wa Makkah na kuletwa kwa Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam, ni watu wachache katika mji wa Makkah waliothubutu kusilimu. Miongoni mwao alikuwa ni Sumayyah. Kwa mujibu wa nukuu za kihistoria anasemekana ni mtu wa saba kusilimu. Alisilimu yeye pamoja na mumewe na mtoto wao ‘Ammaar.

    Kusilimu kwao wakati wakihesabika kuwa wageni kwa kukosa nasaba inayojulikana, familia ya mama Sumayyah ilikuwa katika wakati mgumu.

    Kutoka kwa Mujahid anasema: Wa kwanza kudhihirisha Uislamu ni saba. Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam, AbuBakr, Bilaal, Khabaab, Suhayb, ‘Ammaar na Sumayyah . Ama Mtume Salla Allahu ‘Alayhi alihamiwa na Ami yake Abu Talib. Abu Bakr ilimhami kaumu yake na adhabu, wakachukuliwa wengine na kuvishwa minyororo ya chuma na kupelekwa kwenye jangwa , jua likiwaka na kuteswa haki ya kuteswa….

    Aliposikia Abu Jahl kusilimu kwao pia alikwenda kuwatesa Sumayyah, mumewe na mtoto wao ‘Ammaar kwa kuwapiga wote. Ikumbukwe Sumayyah alikuwa tayari ni mtu mzima. Watu walikuwa wakipita kushuhudia mateso waliyokuwa wakiyapata kwa kulazwa chini kwenye mchanga umoto, huku wakipigwa na jua kali la jangwani kufikia kuzimia na wakiamka tu mateso huendelea wakitakiwa kuikana dini mpya na kurudi katika kuabudu masanamu.

    Siku moja alipita Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam sokoni  na kuona ukatili wa Maquraysh walipokuwa wakiwatesa familia ya Yaasir. Lakini hakuweza kufanya chochote kwa kutokuwa na uwezo na aliwaombea du’aa kwa kusema:

    أَبْشِرُوا آلَ عَمَّارٍ ، وَآلَ يَاسِرٍ ، فَإِنَّ مَوْعِدَكُمُ الْجَنَّةُ  "المستدرك(5666) صحيح

    Nnawabashiria Enyi Ukoo wa ‘Ammaar na ukoo wa Yaasir. Hakika miadi yenu ni pepo.” Al Mustadrak – Sahih

    Ni katika kipindi hiki Waislamu dhaifu wasiokuwa na himaya au kinga kutoka kwa  Maquraysh walipata taabu sana kama kina Bilaal, Suhayb, Khabaab na wengineo.

    Jaribu kufikiria aina ya mateso aliyoyapata Sumayyah ambae ni mwanamke mtu mzima na jinsi alivyokataa kubadilisha imani yake na kuiuza dini yake.

    Siku moja alipita Abu Jahl karibu na sehemu waliyokuwa wakiendelea kuteswa na kumsikia Sumayyah akilirudia neo la Tawhiyd – Ahad Ahad – mmoja, mmoja, Allahu Akbar, Allahu Akbar – Mwenyezi Mungu ni mkubwa Mwenyezi Mungu ni mkubwa. Abu Jahl , kwa hasira na ghadhabu, alimuamrisha amkufurishe Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam. Sumayyah alimkatalia. Na alipokuwa anamkaribia alijikongoja kwa nguvu chache alizokuwa nazo na kumtemea mate Abu Jahl  usoni.

    Si kitu alichokitarajia kufanyiwa sayyid wa Maquraysh na mama huyu aliye chini akiugua kwa mateso na adhabu. Ghadhabu zilimpanda Abu Jahl na kuchukua mkuki ambao alimchoma Sumayyah na kufariki hapo hapo. Sumayyah alikuwa ni Muislamu wa mwanzo kufa shahidi.

    Licha ya kuwa dhaifu, licha ya kutokuwa na nasaba ya kumlinda,Sumayyah alisalimisha maisha yake kwa Allah Subhaanahu Wata’ala na Mtume wake Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam. Hakukubali kumsaliti Mola wake wala kumsaliti Mtume wake. Licha ya kwamba ndiyo kwanza Uislamu unaanza, Sumayyah alionesha na kuwawekea Waislamu msingi na maana ya kushikamana na kujenga msimamo madhubuti katika dini. Ni msingi huu ambao Allah Subhaahau Wata’ala anatukumbusha katika Quraan kwa kusema Attawbah /111

    إِنَّ اللّهَ اشْتَرَى مِنَ الْمُؤْمِنِينَ أَنفُسَهُمْ وَأَمْوَالَهُم بِأَنَّ لَهُمُ الجَنَّةَ يُقَاتِلُونَ فِي سَبِيلِ اللّهِ فَيَقْتُلُونَ وَيُقْتَلُونَ وَعْدًا عَلَيْهِ حَقًّا فِي التَّوْرَاةِ وَالإِنجِيلِ وَالْقُرْآنِ وَمَنْ أَوْفَى بِعَهْدِهِ مِنَ اللّهِ فَاسْتَبْشِرُواْ بِبَيْعِكُمُ الَّذِي بَايَعْتُم بِهِ وَذَلِكَ هُوَ الْفَوْزُ الْعَظِيمُ

    Hakika Allah amenunua kwa Waumini nafsi zao na mali zao kwa kuwa wao watapata Pepo. Wanapigana katika Njia ya Allah - wanauwa na wanauwawa. Hii ni ahadi aliyojilazimisha kwa Haki katika Taurati na Injili na Quraan. Na nani atimizae ahadi kuliko Allah? Basi furahini kwa biashara yenu mliyofanya naye. Na huko ndiko kufuzu kukubwa.

    Alipouawa Abu Jahl katika vita vya Badr , Mtume Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam alimwambia ‘Ammaar bin Yaasir kwamba:

    قتل الله قاتل أمِّك"

    “Allah amemuua (leo) aliyemuua mama yako”

    Sumayyah ni mfano wa kuigwa katika kusadikisha yale waliyoahidi kwa Mola wao litokee lenye kutokea. Ni mfano mwema wa kujifundisha nini maana ya kujiweka katika msimamo imara usiotetereka katika dini. Amesadikisha Allah Subhaanahu Wata’ala aliposema Al Ahzaab/23

    مِنَ الْمُؤْمِنِينَ رِجَالٌ صَدَقُوا مَا عَاهَدُوا اللَّهَ عَلَيْهِ فَمِنْهُم مَّن قَضَى نَحْبَهُ وَمِنْهُم مَّن يَنتَظِرُ وَمَا بَدَّلُوا تَبْدِيلًا

    Miongoni mwa Waumini wapo watu waliotimiza waliyoahidiana na Allah. Baadhi yao wamekwishakufa, na baadhi wanangojea, wala hawakubadilisha (ahadi) hata kidogo.

    No comments:

    Post a Comment

    Fashion

    Beauty

    Culture